 Umeshawahi
 kujiuliza unaweza kuufanyia nini mshahara wa shilingi elfu 60 kwa 
mwezi? Basi usishangae pale unapozidishiwa bili, unapoombwa ofa au 
kutegwa kwa namna yoyote ili utoe fedha zaidi, hii yote huja ili 
kuongezea kipato.
Umeshawahi
 kujiuliza unaweza kuufanyia nini mshahara wa shilingi elfu 60 kwa 
mwezi? Basi usishangae pale unapozidishiwa bili, unapoombwa ofa au 
kutegwa kwa namna yoyote ili utoe fedha zaidi, hii yote huja ili 
kuongezea kipato. 
 
Piga
 hesabu hizi, kodi ya chumba shilingi 15,000, nauli ya daladala kwa siku
 tufanye shilingi 800 kwa siku (inaweza kuwa zaidi kwa wanaopanda mabasi
 manne kwa siku) , kilo moja ya unga 900, sukari shilingi 2,000 ukipiga 
na mahitaji mengine muhimu unaweza kuona hii shilingi elfu 60 inaisha 
ndani ya siku mbili tu.
 
Sasa
 je wanamudu vipi gharama za maisha ambazo zinapanda kila kukicha? Salma
 Chitenga (Sio jina lake halisi) anasema kila kazi ina mbinu zake; kwani
 kila mbuzi hula kwa urefu wa kamba yake.
 
Anasema
 yeye na wenzake sita wanaishi katika chumba walichopewa na mmiliki wa 
baa anayoifanyia kazi iliyopo maeneo ya External jijini Dar es Salaam.
 
“Ninaishi 
 katika chumba tulichopewa na mmiliki wa baa ninayoifanyia kazi ( 
mwenyewe analiita ‘ghetto’) akisema kuwa fedha anazolipwa zinamsaidia 
kujikimu na kusaidia ndugu zake waliopo kijijini.
 
“Ninalipwa
 shilingi 60,000 kwa mwezi, lakini kila siku ninapewa shilingi 1,500 kwa
 ajili ya chakula, pia tajiri ametupa chumba tunaishi hapa, fedha 
ninayopata ninanunua nguo na pia kiasi kidogo huwa ninamtumia mama yangu
 kijijini,” anasema Salma.
 
Aisha
 Suleiman ni mfanyakazi wa baa na ni mama wa mtoto mmoja wa kiume mwenye
 umri wa mwaka mmoja na nusu. Yeye anasema changamoto yake kubwa iliyo 
mbele yake ni jinsi ya kuibana fedha ndogo anayoipata.
 
“Nina
 mtoto mdogo ambaye anahitaji matunzo na mshahara wenyewe ni duni, 
inabidi nitumie mbinu mbalimbali kujiongezea kipato,” anasema Aisha.
 
Aisha
 anasema zipo njia nyingi za kujiongezea kipato ambazo wafanyakazi wa 
baa huzitumia huku akisisitiza kuwa zipo mbaya na nzuri.
 
Anakiri
 kuwa mshahara wa shilingi 60,000 ni mdogo hasa kwa mtu mwenye familia 
kama yeye kwani lazima apange chumba na aache hela ya chakula kila siku.
 
“Kwa
 kuwa kazi zangu ninafanya usiku, inabidi katika hiyo fedha ninunue na 
maziwa ya mtoto pia nimuachie fedha kidogo mtu anayenitunzia mtoto wangu
 wakati sipo, nimeshindwa kuajiri mfanyakazi wa ndani kwa kuwa kipato 
changu ni kidogo,” anasema Aisha.
 
Waswahili
 wanasema njaa huleta akili na hivi ndivyo anavyosimulia Aisha akisema 
kuwa msukumo wa kutafuta fedha zaidi umetokana na majukumu aliyonayo kwa
 familia yake “Kuna njia nyingi za 
kujiongezea kipato, mfano ukipata wateja na kuwapa huduma nzuri hawawezi
 kuondoka bila kukupa chochote au hata ofa ya kinywaji,” anasema na 
kuongeza.
“Ukiwa
 mkarimu kwa mteja, hasa wanaume, anaweza kukupa ofa ya bia, hapo ni 
ujanja wako sasa ‘kucheza’ ili ile ofa usiinywe na badala yake uchukue 
fedha kwasababu wateja wengine akikupa bia anakulazimisha uinywe,” 
anasema Aisha.
 
Aidha
 anasema hategemei ofa za bia peke yake, anapohudumia wateja vizuri pia 
humpa kitu kidogo maarufu kwa jina la ‘tip’ akisema hizo pekee kwa siku 
kama mambo yakienda vizuri anaweza kupata hata Sh 5,000.
 
Hii
 ni sehemu tu ya maisha ya wafanyakazi wa baa, wapo ambao hulipwa 
kutokana na huduma waliyotoa kwa siku, wapo ambao hulipwa kwa kuongeza 
bei ya kawaida ya vinywaji ya baa husika, lakini wapo ambao hujilipa 
wanavyojua wenyewe.